Google ni 
ulimwengu wa uvumbuzi wa bidhaa na majaribio ya teknolojia, katika 
baadhi ya mawazo na uvumbuzi ambao Google wanaendelea kufanyia kazi kuna
 mambo ambayo sio ya kufikirika, gari inayojiendesha na kompyuta ya 
kuvaa kama miwani ni miongoni mwa teknolojia hizo, kwa mtazamo wa haraka
 unaweza kudhani kuwa itachukua miaka zaidi ya 10 Google kuweza kuziuza 
bidhaa hizo kwa watu wa kawaida.
Ukweli
 ni kwamba Google imeshatangaza kuwa Google Glass itaanza kuuzwa mwaka 
huu wa 2013. Google Glass ni kompyuta ambayo huvaliwa kama miwani na ina
 uwezo na matumizi mbali mbali kama vile kurekodi video na kupiga picha.
 Katika ongezo jipya la Google Glass ni kwamba kompyuta hiyo itaweza 
kutumia amri za sauti (voice command), kuanzisha amri ya sauti unatakiwa
 kuiambia miwani hiyo “OK Glass” na miwani itaanza kukusikiliza unataka 
ifanye nini kabla ya kuipa amri kama vile “record video”. Pia Google 
wameonyesha baadhi ya matumizi ya miwani hiyo ambayo ni ya kawaida 
kabisa mbali na yale ya kuchupa na parashuti kutoka kwenye ndege. 
Matumizi hayo 
ni pamoja na kurekodi video na kupiga picha wakati wa kuendesha gari, 
unapocheza tenis na wakati wa kupanda mlima, pia Google imeonyesha 
matumizi ya Miwani  kwa wapanda pembea na wacheza muziki. Miwani hii 
huenda ikatufanya Waswahili wengi zaidi kuamua kuupanda Mlima wa 
Kilimanjaro. Pia Google glass itaweza kutoa taarifa kama vile urefu wa 
barabara unayotembea, ni wakati gani ndege inatarajiwa kutua uwanjani, 
kutafsiri maneno kutoka lugha moja kwenda nyingine na kukwambia 
umesimama mtaa gani na hata kukuelekeza njia. Kwa kifupi Google 
wanaelekea kuipa miwani hiyo uwezo wa “Google Now” ambayo ni search 
engine inayotumia maneno.
Google
 tayari imeanza kuwauzia miwani hiyo watengeneza apps (developers) ili 
waweze kuanza kutengeza apps za miwani hii kwa matumizi mbali mbali. 
Miwani hiyo itawagharimu developers jumla ya $1,500.00, kwa miwani moja 
ambazo ni sawa na fedha taslimu za Kitanzania 2,451,000. Google pia 
imethibitisha kuwa miwani hiyo itakuwa na Apps za simu na tablet za iOS 
na Android ili kuweza kushirikiana na gajeti hizo katika utendaji wa 
mambo mbali mbali kama vile ku-send message.
Ingawa
 teknolojia hii ni mapema mno kujua itakuwa na uwezo na matumizi ya aina
 gani hasa mbali na haya machache tuliyoyaeleza, wengi miongoni mwa 
developers wanaelekewa kuvutiwa nayo kwa kiasi kikubwa. Google pia 
imeanzisha mashindano kwa watu binafsi kuwaandikia twitter au Google+ 
kueleza ni jinsi gani miwani hii itatumika. Miongoni mwa masharti ya 
shindano hilo ni kuwa maneno yasizidi 50, video isizidi sekunde 15, 
picha zisizozidi 5 na utumie hashtag #ifihadglass. Kisha unatakiwa 
ufuatilie Google+ (+ProjectGlass) au Twitter (@projectglass)
 na Google imeahidi kujibu direct message kwa washindi. Zawadi kwa 
washindi ni kuwa kupata nafasi ya kuinunua miwani hiyo mapema, hivyo 
ukishinda uweke tayari T Sh. Milioni mbili na nusu.




