Uvumi
na minong’ono ni mambo ambayo hayaachani na kampuni ya Apple yenye
makao makuu yake huko Cupertino. Baada ya uvumi kwamba Apple wangetoa
televisheni mwaka huu kuanza kufifia, sasa hivi kuna minong’ono kwamba
kampuni hiyo itatoa saa ya mkononi yenye kutumia iOS. Bloomberg
imetangaza kwamba kampuni hiyo inatatoa saa ambayo wameipa jina la
kubuni la iWatch mwaka huu, ambapo imeripotiwa kwamba Apple tayari ina
wafanyakazi karibu 100 wanaoshughulikia gajeti hiyo.
iWatch
inasemekana kuwa itakuwa na uwezo wa kushirikiana na gajeti za Apple
zinazotumia iOS hivyo kwa kutumia saa hiyo unaweza kupiga simu, kutuma
ujumbe mfupi (SMS), kusikiliza muziki, kuseti miadi kwenye kalenda au
kuitumia kama pedometa, kifaa ambacho ni muhimu kwa wanamichezo mbali
mbali. Iwapo saa hiyo itatoka basi itaboresha usalama katika maeneo
yenye matatizo ya uporaji wa simu kwani hutakuwa na haja ya kutoa simu
yako wakati umevaa saa hiyo ili kupiga simu au kufanya matumizi mbali
mbali, ingawa tayari unaweza kufanya hivyo kwa kutumia huduma ya app ya
Siri na earpods.
Apple
ambayo inahitaji gajeti mpya ili kuweza kunyanyua tena thamani ya hisa
zake ambazo tangu mwaka jana zimekuwa zikiteremka thamani, imeelezwa
kuwa itaweza kupata faida kubwa katika biashara ya saa kuliko
televisheni. Kwa mujibu wa mchambuzi wa City Group Bwana Oliver Chen
amedai Apple itaweza kuongeza jumla ya $6 bilioni katika mapato yake
iwapo bidhaa hiyo itakubalika na watumiaji gajeti za iOS yaani iPad,
iPhone, iPod Touch na Apple TV.
Uvumi
huu unazidi kupata nguvu kwa vile miongoni mwa haki miliki 79 mpya
zilizosajiliwa na kampuni ya Apple zipo zinazohusiana na saa ya mkononi,
pia itakumbukwa kuwa iPod Nano toleo la mwaka 2010 ilikuwa inaweza
kutumika kama saa ingawa iPod Nano hiyo haikuwa inatumia iOS. Vile vile
saa hiyo inatarajiwa kuwa na sensa viunganishi mbali mbali kama vile
bluetooth, akselerometa na GPS.
Hivi
karibuni kumekuwa na gajeti mbali mbali za kuvaa mkononi ambazo
zimekuwa zikiuzwa kwa $100 au zaidi, gajeti hizo ni kama vile Nike Fuel
Band na Fitbit Zip Wireless, bila ya shaka hivi vimewapelekea Apple
kuona kwamba kuna nafasi kubwa ya wao wenyewe kutoa gajeti kama hizi
ambapo ikitumia iOS itakuwa na muingiliano mkubwa zaidi na simu, tablet
pamoja na iPod zao.
Huko
nyuma Apple ilikuwa ni kampuni ambayo inasifika kwa kuweza kuhifadhi
siri za gajeti zao mpya hadi inapofikia uzinduaji rasmi, hivi karibuni
gajeti mbali mbali zimekuwa zikivuja na kujulikana habari zake kabla ya
Apple kuzitangaza rasmi, mfano mzuri ni pale picha ya iPhone 5
iliposambaa mitandaoni kabla ya simu hiyo kutangazwa na kutolewa rasmi.
Iwapo saa hii itatolewa basi huenda ikaleta mapinduzi makubwa katika biashara ya saa. Biahsara ambayo imefifia kwa kiasi kikubwa kwa vile watu wengi hawaoni tena umuhimu wa kuvaa saa kutokana na simu zao kuwa na uwezo wa kuwajulisha wakati. Itakuwa ni faraja kwa kampuni zinazotengeneza simu kwani soko litaimarika lakini pia itakuwa ni changamoto kubwa kwa wazalishaji hao kuweza kuinua viwango vya saa zao na kuifikia iWatch.
Iwapo saa hii itatolewa basi huenda ikaleta mapinduzi makubwa katika biashara ya saa. Biahsara ambayo imefifia kwa kiasi kikubwa kwa vile watu wengi hawaoni tena umuhimu wa kuvaa saa kutokana na simu zao kuwa na uwezo wa kuwajulisha wakati. Itakuwa ni faraja kwa kampuni zinazotengeneza simu kwani soko litaimarika lakini pia itakuwa ni changamoto kubwa kwa wazalishaji hao kuweza kuinua viwango vya saa zao na kuifikia iWatch.