Miongoni mwa masharti ya Windows 8 ambayo yaliwekwa na Microsoft ni kutoruhusu tablet zenye rezolushani chini ya 1366 x 768, lengo la Microsoft likiwa ni kuhakikisha kwamba wanotoa ushindani katika ubora wa tablet. Hii imesaidia kwa tablet za Windows 8 kuwa nzuri kiasi fulani lakini Microsoft wamefanya kosa la kimkakati kwani kuna mfumuko mkubwa wa mauzo ya tablet kati ya7” na 8” kufuatia mafanikio makubwa ya bidhaa kama vile iPad Mini, Amazon Kindle Fire na Nexus 7. Rezolushani za juu kabisa katika tablet za 7" ni zile zilizotumika kwenye Kindle Fire HD na Nexus 7 ambazo zote zina 1280 x 800. (216ppi), hizi zimepungua kwa 1.2% kufikia kiwango ambacho Microsoft walikitaka awali, ambapo iPad Mini ina 1024x768 (163ppi), hivyo kwa viwango vya Micrososft iPad Mini iko chini sana. 
Baada ya kugundua kosa hilo Microsoft wameregeza masharti ya Windows 8 na hivyo kwa sasa tablet ndogo na za rezolushani za chini zitaruhusiwa. Hivyo tutarajie tableti ndogo za Windows 8 kwenye robo ya mwisho ya mwaka huu au mapema mwakani. Extreme Tech wakiripoti taarifa hiyo ya Microsoft wameeleza kwamba taarifa hiyo imefuatiwa marekebisho katika taratibu na sheria za kuruhusiwa (Certification rules) kutumia Windows 8, hata hivyo hii itakuwa kwa tolewa la Windows 8 RT peke yake. Faida kubwa ya udogo huu ni urahisi wa bei. Hata hivyo tablet hizi zitatumia Windows RT tu na hakutakuwa za Windows Pro, kitu ambacho hakiingia akilini kwa vile cha msingi ni nguvu ya tablet na si ukubwa wa tablet.


Kwa msingi huu Microsoft bado wanaonekana wamechanganyikiwa na hivyo kujiwekea vikwazo vya kimaendeleo wenyewe. Baada ya ukiritimba wa muda mrefu kibiashara kwa sasa Microsoft hawako katika hali nzuri, hii ikiwa ni pamoja na kufanya jitihada kubwa za kuleta mabadiliko katika bidhaa muhimu za kampuni hiyo na hasa OS za kompyuta, tablet na simu. Hisa za Windows Phone kulinganisha na OS nyingine ni 6% kwa mujibu wa repoti ya Mintel, hisa ya Windows 8 katika soko la tablet kwa mujibu wa ripoti ya IDC ni 2%, mauzo ya PC yanaendelea kuzorota mwaka hadi mwaka. 

Hata hivyo Microsoft wako mbali na kukata tamaa na hasa katika simu na tableti, hivi karibuni wamefanya uboreshaji wa Windows 8 na programu kama vile za Mail, People na Kalenda zimepata sura mpya, pia jarida la Tech linalotolewa na T3 limeripoti kwamba Microsoft wako jikoni wakitayarisha Windows mpya ambayo imepewa jina la muda (codename) Windows Blue, Windows hii huenda ni sehemu ya mpango wa Microsoft wa kuziunganisha Windows Phone 8, Windows RT na Windows 8 Pro kuwa moja na pia kujitayarisha katika wakati wa kuachana na PC.

Darrell Etherington wa Tech Crunch akizungumzia Windows Blue baada ya kuijaribu ameonekana kuvutiwa mno na alichokiona, amesema “Microsoft inaelekea kutumia uzoefu wake wa UI mpya kuachana na mtindo wa kizamani wa desktop.” Windows Blue tayari umeshavuja na kujaribiwa na watu kadhaa, naye Paul Thurrott wa mtandao wa WinSuperSite amesema apps za Windows Blue zinathibitisha kwamba Windows inaachana na masuala wa desktop ambapo yeye anaamini kwamba Windows Blue hatimae ndio itakuja kuwa Windows 9. 

Ni mapema mno kuanza kuzungumzia Windows nyingine kwa vile Windows 8 bado ni mpya, hata hivyo Windows 8 inakabiliwa na kukosolewa hapa na pale huku raisi wa Samsung kitengo cha Memory Chip bwana Jun Dong-soo akiifananisha Windows 8 na Vista, Vista ni toleo linaloonekana kuwa Windows walikwenda mchomo, na hivyo haikukaa muda mrefu kabla ya kutoka mpya yake, je Windows kuharakisha na toleo la Blue kunatokana na kuwa wameshaona matatizo ya Windows 8? Nivigumu kulipata jibu la swali hili kwa sasa. 

Hata hivyo hatuishi tena katika ulimwengu wa kusubiri miaka 3 kabla ya kutoa toleo jipya la OS. Apple katika kipindi cha Miaka mitatu iliyopita wametoa matoleo matatu tofauti ya Mac OSX yaani Snow Leopard, Lion na Mountain Lion. Nazo OS na simu na tablet kama vile Android na iOS hutoka toleo jipya karibu kila mwaka. Hivyo huenda Microsoft wameamka kutoka kwenye usingizi mzito wa kuacha OS kukaa miaka 3 au zaidi. 
SHUKA CHINI KUTOA MAONI YAKO
 
Top